Saturday, April 28, 2012

TANROADS YASAINI MKATABA WA TSH BILIONI 12.34 UJENZI WA DARAJA LA MBUTU

Na Ismail Ngayonga

MAELEZO

Dar es Salaam


SERIKALI kupitia Wakala wa Barabara Nchini (Tanroads) imesaini mkataba na makampuni 13 ya wakandarasi wa ndani kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Mbutu lililopo katika Wilaya ya Igunga mkoani Tabora.

Akizungumza kabla ya utiaji saini mkataba huo jana (juzi), Mtendaji Mkuu wa Tanroads Mhandisi Patrick Mfugale alisema ujenzi wa daraja hilo utagharimu kiasi cha Tsh. Bilioni 12.34 na unataraji kukamilika mwezi Septemba mwaka 2013.

Alitaja wakandarasi hao 13 waliounda umoja wa ujenzi wa mradi daraja hilo kuwa ni Skol Building Contractors Ltd, Del Monte (T) Ltd, Mayanga Contractors Company Ltd, Casco Construction Ltd, Electrics International Company Ltd, Kika Construction Company Ltd.

Wakandarasi wengine ni Gemen Engineering Company Ltd, Milembe Construction Company Ltd, Lukolo Company Ltd, Mac Contractors Co. Ltd, Nyakirang’anyi Construction Ltd, Nyegezi J.J Construction Ltd na Concrete Meters Company (T) Ltd.

Mhandisi Mfugale aliwataka wakandarasi kujenga daraja hilo katika ubora na viwango walivyojiwekea kwani la Serikali la kuwatumia wakandarasi ni pamoja kupunguza gharama za miradi ya ujenzi wa barabara na pia kutoa kipaumbele kwa wakandarasi wazalendo.

Akifafanua kuhusu ujenzi huo, Mhandisi Mfugale alisema daraja hilo litajengwa kwa zege la simenti na litakuwa na urefu wa mita 40 na upana wa mita 10.7. “Daraja litakuwa na uwezo wa kubeba uzito wa juu kabisa unaokubalika kisheria hapa nchini ambao ni tani 56” alisema.

Aidha alisema kuwa mradi huo pia utahusisha ujenzi wa makaravati 7 ya zege yenye upana wa mita 8 hadi 14 pamoja na ujenzi wa tuta la barabara lenye urefu wa kilomita 3 kwa kiwango cha changarawe.

Kwa mujibu wa Mhandisi mfugale alisema matarajio ya Serikali ya kutekeleza mradi huo ni kuhakikisha kuwa panakuwapo mawasiliano ya uhakika ya barabara katika vipindi vyote vya mwaka kati ya vijiji vilivyopo katika tarafa ya Igurubi yenye wakazi zaidi ya 94,449 na mji wa Igunga.

Kukamilika kwa mradi huu kutachochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Igunga ambao hujishughulisha na kilimo cha mazao ya biashara na chakula yakiwemo pamba, mahindi, mtama, viazi na dengu.

Kwa upande wake, Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mhandisi Dk. John Ndunguru alisema Serikali ilianza kutenga fedha ya ujenzi wa mradi huo katika mwaka wa fedha 2011 na kuikamilisha katika mwaka wa fedha 2012.

Aidha Dk. Ndunguru aliitaka Tanroads kusimamia kwa karibu kazi ya ujenzi huo na kuhakikisha kuwa inafanywa kwa ubora na kuzingatia muda uliowekwa.

“Ni matumani yangu kuwa malengo yaliyokusudiwa ya utekelezaji wa mradi, ambayo ni kuimarisha mawasaliano ya barabara kwa vipindi vyote vya mwaka yatafikiwa’’ alisema Dk. Ndunguru.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili wa Wakandarasi Nchini CRB), Bi. Consolata Ngimbwa aliishukuru Serikali kwa kusikia kilio cha wakandarasi wazalendo na kuahidi bodi itawasimamia wakandarasi hao ili kuhakikisha kuwa kazi ya ujenzi huo itafanyika katika viwango vinavyotakiwa.

“Wakandarasi wenzangu mmepewa fursa ambayo wengine waliitaka na hamna budi kutambua kuwa wenzetu wapo nyuma yenu kutazama kile mnachokifanya” alisema.

Mwaka 2006 mvua kubwa ilinyesha Wilayani Igunga kuharibu madaraja ya Mbutu na hivyo kukatisha mawasiliano kati ya tarafa za Igurubi na makao makuu ya Wilaya ya Igunga.

No comments: