Friday, October 5, 2012

NAIBU WAZIRI WA UJENZI AIAGIZA TEMESA KUBORESHA HUDUMA.


Naibu Waziri wa Ujenzi Mhe. Gerson Lwenge (katikati) akionyeshwa na Mtendaji Mkuu wa TEMESA, Eng. Marcelin Magesa (kulia) maendeleo ya ujenzi wa kivuko cha Msanga mkuu kama unavyoendelea kutekelezwa eneo la Kurasini jijini Dar es Salaam. Kushoto mbele ni Eng. Rajab Ngome,  Mkurugenzi Msaidizi wa Ufundi kutoka Wizara ya Ujenzi.
Mhe. Naibu Waziri wa Ujenzi  Gerson  Lwenge leo amefanya ziara ya kikazi kutembelea Wakala wa Ufundi na Umeme TEMESA. Katika ziara hiyo Mhe. Lwenge amewaasa wafanyakazi pamoja na Menejimenti ya TEMESA kufanya kazi kwa weledi pamoja na moyo wa kutuma zaidi ili Wakala huo uweze kufanikiwa katika majukumu yake.
Mhe.Naibu Waziri ameitaka TEMESA kuangalia vyanzo vingine vya mapato, ikiwa ni pamoja na kuongea na Taasisi za Fedha ambazo zinamasharti nafuu ya mikopo ili kuongeza mtaji wake. Aidha, Naibu Waziri amehaidi kulivalia njuga suala la madeni ambalo taasisi hiyo imekuwa ikizidai Wizara na Idara mbali mbali za Serikali, hata ikibidi kuongea na Hazina ili fedha za madeni hayo zikatwe moja kwa moja kutoka Hazina. Vile vile ameitaka TEMESA kujenga hoja kwa vivuko ambavyo vinaendeshwa kwa hasara ili Serikali iangalie gani inaweza kuwasidia hata kupitia kwenye Halmashauri husika.
Aliongelea usafiri wa boti kati ya Dar na Bagamoyo Mhe. Naibu Waziri ameiomba TEMESA kuharakisha mchakato huo ili huduma hiyo iweze kuanza mara moja.
Awali akimkaribisha Mhe. Naibu Waziri kuongea na Wafanyakazi, Mtendaji MKuu wa Temesa Eng. Marcelin  Magesa alizitaja changamoto mbali mbali zinazokabili wakala huo ikiwa ni pamoja na kutolipwa madai yao kwa wakati, kwa huduma zinazotolewa na TEMESA. Upungufu wa watumishi kutokana na wengi kustaafu na wengine kufariki na kuwa mchakato wa Serikali unachukua muda mrefu. Changamoto nyingine ni kuwepo kwa mapato kidogo kwenye baadhi ya vivuko kiasi cha kutokidhi gharama za uendeshaji. Mtendaji Mkuu huyo wa TEMESA ameiomba Serikali iangalie uwezekano wa kuipatia taasisi hiyo mtaji ili imudu kukabiliana na changamoto hizo pamoja na ubovu wa karakana na uhaba wa vitendea kazi katika karakana zote nchini zinazo simamiwa na TEMESA
Wakati huo huo akizungumzia suala la Dar – Bagamoyo ferry Mtendaji Mkuu alisema tayari Wizara ya Ardhi imeshatoa Ramani kwa ajili ya maeneo ya maegesho na tenda kwa ajili ya kumpata Mhandisi Mshauri zimefunguliwa jana Jumatano tayari kwa kuanza kazi  hiyo.
Taarifa Hii imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma
Wizara ya Ujenzi

No comments: