Wednesday, May 2, 2012

Duni Wa CUF Akiri; Wengi Wamevunjika Moyo

Watu hawana imani na sisi kabisa!!!!!!!!!!!!!!

( Pichani; Mheshimiwa Duni akiwa na mwandishi wa habari hii Bw. Saidi Yakubu)
JUMA DUNI AKIRI WANACUF WENGI WAMEVUNJIKA MOYO BAADA YA UCHAGUZI.
Na Saidi Yakubu, London, Uingereza
Naibu Katibu wa chama cha CUF, amekiri kwamba baada ya uchaguzi wamekuwa na kazi ngumu ya kuendelea kuhamasisha wafuasi wa chama hicho ambao wengi wameonekana kuvunjika moyo.
Bwana Duni aliyasema hayo alipokuwa akihutubia takriban watanzania 200 mjini London wengi wao wakiwa na asili ya Zanzibar. Mkutano huo uliandaliwa na Jumuiya ya Zanzibar Welfare Association ZAWA. Bwana Duni alisema ni haki ya wanachama wao kuvunjika moyo lakini alitoa kwamba wasikate tamaa kwani chama kinajizatiti kutafuta njia bora za kutatua mtafaruku wa Zanzibar, ‘’Tuliamua kukaa kimya baada ya uchaguzi kwa makusudi lengo letu lilikuwa ni kutafakari na kutathmini hali ya mambo, sasa hivi nikiwa huku kuna taarifa kwamba CCM wanataka tukutane nao tena, nasi tutakwenda na kubwa la kuanzia ni kuwauliza kwa vipi safari hii tuwaamini ilhali miafaka miwili haikutekelezwa’’ alisema.Kiongozi huyo alikuwa na wakati mgumu kujibu maswali ya waliohudhuria ambao wengi wao walionyeshwa kutoridhika na muelekeo wa chama baada ya uchaguzi ‘’Tumepokonywa ushindi mara mbili, watu wetu wameuwawa, viongozi waliohusika wamekwishastaafu na wengine wapo madarakani, baadhi yetu tumekuja huku kukimbia hali ya nyumbani ilivyokuwa lakini mnachofanya ni kuongea nao, sisi tunataka hatua za kisheria zichukuliwe kwa wahusika wafikishwe mahakamani kama sio nyumbani basi THE HAGUE, kama wameweza kumpeleka Saddam kwanini wasipelekwe hawa wa kwetu?’’ alihoji Bwana Ali kutoka Leicester. Hata hivyo akijibu hoja hizo Bwana Duni alikariri kauli yake kuwa, kwa vile wameitwa katika mkutano wa sasa na CCM wamemtuma Katibu Mkuu Makamba kuandaa taratibu za mazungumzo ya sasa, itakuwa si busara kususia,’’Sisi tunaamini Kikwete anaweza kutatua hili la Zanzibar ni uamuzi tu na tunashukuru jitihada tunaziona, sasa tunasema apewe muda’’ aliongeza Bwana Duni.
Akizungumza na Mwandishi wa habari hizi aliyetaka kujua iwapo wakati umefika sasa kwa yeye kumrithi Maalim Seif katika nafasi ya mgombea urais wa Zanzibar kwa mwaka 2010, Bwana Duni alikataa kuweka wazi iwapo hilo linawezekana au la, ‘’Sisi kama chama tuna taratibu zetu, Mwaka 1995 nilikuwa mgombea mwenza, mwaka 2000 uchaguzi unafayika nilikuwa jela na mwaka jana nikawa tena mgombea mwenza, nimepewa madaraka mapya sasa kuwa mkurugenzi wa chama wa fedha hivyo ni utaratibu tu, lakini kuhusu mimi binafsi nadhani ni mapema sasa kusema nitakubali au la’’. Akizungumzia mwaka mmoja wa Rais Kikwete Bwana Duni Haji alisema umekuwa ni mwaka akiwa amejitahidi sana kurekebisha hali ya mambo yalivyo ingawa bado ana kazi kubwa, ‘’Ameonyesha kwamba anaweza kuchukua maamuzi mazito kama kiongozi, kulikuwa na mauaji Dar es salaam ameweza kuunda tume, ilipompelekea ripoti akaisoma na kuagiza wahusika wachukuliwe hatua, hivi sasa Polisi mkubwa alietajwa ZOMBE, sasa hivi amesimamishwa kizimbani, hii ni nzuri kwa kiongozi manake mauaji ya 2001, Mkapa aliunda tume ya uongo ya Hashim Mbita mpaka leo hakuna lolote lililofanyika, lakini nimeshasema sana kumwambia Mheshimiwa Kikwete hili la Zanzibar alisimamie vizuri’’.

No comments: