Thursday, October 11, 2012

VITUKO UWT ,MGOMBEA AKATAA MATOKEO BAADA YA KUSHINDWA NJOMBE

Scolastca Kevela akisaini fomu ya kukataa matokeo

ALIYEKUWA mgombea wa nafasi ya Uenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania(UWT) wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Njombe, Scolastica Kevela juzi alionja machungu ya siasa za makundi baada ya kuzomewa kwa nguvu na baadhi ya wajumbe wa mkutano huo.
Katika uchaguzi huo ulioonekana kugubikwa na muelekeo wa siasa za Uchaguzi Mkuu wa 2015, Rosemary Lwiva aliibuka mshindi kwa kujipatia kura 190, huku Kevela akipata kura 164.
Lwiva ambaye hata hivyo hakuweza kuthibitisha taarifa hii, anadaiwa kuwa katika moja ya kundi la wabunge wanaotaka kujisafishia njia ya uteuzi wakati wa mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa 2015 huku Kevela akionekana kuwa katika kundi linalotaka kupanua uwanja wa ushindani katika uchaguzi huo kwa kuziunga mkono sura mpya.
Kuwepo kwa muelekeo wa siasa za makundi katika uchaguzi huo kwa kiasi fulani kulidhihirishwa na uwepo wa baadhi ya wabunge wa kiume (majina yanahifadhiwa) ambao mkutano huo ulikuwa hauwahusu moja kwa moja.
Taarifa zilizokuwa zimezagaa ndani na nje ya ukumbi wa UWT ulipofanyika mkutano huo mjini hapa na ambazo zilikanushwa vikali zilidai kwamba mmoja wa wabunge hao aliyekuwa akimfanyia kampeni mmoja wa wagombea hao alikamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kuambana na Rushwa (Takukuru).
“Hizi taarifa sio za kweli hata kidogo, zinaenezwa na wapambe wa mmoja wa wagombea anayejua atashindwa katika uchaguzi huu,” alisema mmoja wa wapambe wa mbunge huyo.
Alisema baada ya kusikia taarifa za mbunge huyo kukamatwa walilazimika kwenda naye katika eneo la mkutano huo ili wale waliokuwa wakivumisha taarifa hizo kwa lengo la kubadili mtazamo wa wajumbe juu ya uchaguzi huo waishiwe hoja.
“Tumekuja naye katika ukummbi wa mkutano huu kama unavyoona, hii ni kudhihirisha kwamba taarifa zilizokuwa zinaenezwa dhidi yake zilikuwa propaganda,” alisema.
Tukio hilo la Kevela kuzomewa lilitokea mara baada  ya mgombea huyo kupewa nafasi ya kuwashukuru wajumbe baada ya matokeo kutangazwa, majira ya saa 1.30 usiku.
Kevela aliyeanza kwa kuwaomba radhi wanawake wenzake alisema hakubaliani na matokeo hayo kwasababu mgombea mwenzake aliyeshinda kiti hicho alitoa rushwa.
“Sio kwamba siwaheshimu, mmeona nimetumia muda kujaza fomu ya kukubali au kukataa matokeo, ukweli ni kwamba huyu mwenzangu aligawa vitenge kwa wajumbe wa Makete na Ludewa…” alisema na kabla hajamaliza wajummbe walisimama na kuanza kumzomea.
Zomea zomea hiyo iliyodumu kwa dakika tatu ilimlazimu Kevela aliyeonekana kupandwa na hasira kumalizia kwa kusema asanteni na kwenda kukaa nyuma ya meza kuu.
Alikuwa Mwenyekiti wa CCM  Mkoa wa Iringa na Njombe anayemaliza muda wake, Deo Sanga aliyetuliza jazba za wajumbe na mgombea huyo.
“Ndugu zanguni hili ndio jeshi litakalotuwezesha kushinda uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2014 na uchaguzi mkuu wa 2015,” alisema.
Sanga ambaye pia ni Mbunge wa Njombe Kaskazini alisema baada ya uchaguzi huo wanawake wanatakiwa kuwa kitu kimoja kwa kujenga mshikamano na kuimarisha umoja wao.
“Vinginevyo tutajiweka katika mazingira ya kushindwa vibaya katika chaguzi hizo zijazo na kama manavyojua katika maeneo mengi ambayo wapinzani wameshinda imetokea hivyo kwasababu ya mgawanyiko wetu,” alisema.
Pamoja na kutoa rai hiyo, Kevela alisema pamoja na kukataa matokeo hayao ndani ya siku 14 atakata rufaa kupinga matokeo hayo kwasababu yaligubikwa na dosari nyingi.(Frank Leonard Blog)

No comments: